0



Mwanamuziki mashuhuri duniani Jennifer Lopez, amejiondoa katika shamra shamra za ufunguzi wa fainali za kombe la dunia ambazo zitafanyika mjini Sao Paulo siku ya Al-khamisi, kabla ya mchezo wa kwanza fainali hizo ambao utashuhudia wenyeji Brazil wakicheza dhidi ya timu ya taifa ya Mexico.
 
Taarifa za mwanamuziki huyo kutoka nchini Marekani zimethibitishwa na shirikisho la soka duniani FIFA, ambapo hata hivyo sababu za kujiondoa kwa Jennifer Lopez hazijaelezwa kwa kina
 
Lopez, alitarajiwa kushiriki katika shamra shamra hizo akiwa sambamba na mwanamuziki wa miondoko ya rap, Pitbull pamoja na Claudia Leitte kutoka nchini Brazil, kwa ajili ya kuimba wimbo maalum wa fainali za kombe la dunia za mwaka huu ambao unaitwa "We Are One,”
 
"Kufuatia sababu zilizo nje ya uwezo wetu, hatutokuwa na Jennifer Lopez, ambae ni mmoja wa wana muziki ambao wamerekodi wimbo maalum wa fainali za mwaka huu, ambao unatarajiwa kuwa sehemu ya ufunguzi.” Imeeleza taarifa ya FIFA.
 
Wasanii 600 wa fani mbali mbali za burudani, wanatarajiwa kushiriki katika shamra shamra za ufunguzi wa fainali za kombe la dunia kwa mwaka huu.
 
Watu zaidi wa elfu sitini (60,000) wanatarajia kushudia shamra shamra za ufunguzi wa fainali za kombe la dunia wakiwa katika uwanja wa Sao Paulo, na wengine zaidi wataziona shughuli hiyo kupitia luninga katika viwanja vya wazi nchini Brazil.

Post a Comment

 
Top