Waziri Mkuu Mizengo Pinda anasema ikiwezekana Kanuni za Kudumu za Bunge zirekebishwe ili kuwabana wabunge wa Upinzani wanaotoka bungeni.
Aidha,
amewataka wabunge kuheshimu mamlaka ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za
Serikali (CAG) na kumwachia jukumu la kufanya ukaguzi kuhusu suala la malipo
kwa Kampuni ya IPTL.
Waziri
Mkuu Pinda aliyasema hayo juzi jioni wakati alipopewa fursa na Spika Anne
Makinda kuzungumza muda mfupi baada ya kupitishwa kwa bajeti ya Wizara ya
Nishati na Madini kwa mwaka 2014/15.
“Kama
inawezekana basi Kanuni zingeweza kurekebishwa, maana jambo hili sio zuri hata
kidogo,” alisema Waziri Mkuu na kushangiliwa na wabunge ambao wengi walikuwa ni
wa Chama Cha Mapinduzi, na wachache wa upinzani waliobaki.
Wabunge
wa Upinzani wakiongozwa na Kiongozi wao, Freeman Mbowe walitoka bungeni juzi
jioni, wakisusa bajeti ya Nishati na Madini kwa madai kuwa wabunge wa CCM
walikuwa wamejipanga kuipitisha, na hivyo kushiriki kwao ni 'kulinajisi Taifa'.
Waziri
Mkuu alisema inamuumiza sana kwa sababu asubuhi wabunge hao wa Upinzani
walishiriki kikao, na kutoa maoni yao, tena kwa maneno mengi.
“Kwa
kweli mimi kinaniumiza sana, asubuhi walikuwapo, wakatoa maneno yao, halafu
jioni watu hawa eti wanatoka nje,” alisema Pinda na kuongeza:
“Hizo
ni dalili za kushindwa hoja, wakaona njia rahisi ni kutoka. Mnyika (John)
alisema maneno mengi hapa, akapiga blah blah kwa kusoma vichwa vya habari. Sasa
baadaye wanatoka. Jibu lake si kutoka.
“Mheshimiwa
Spika, tabia hii inazidi kuongezeka, kama inawezekana, basi Kanuni
zingerekebishwa, kwa sababu jambo hili sio vizuri hata kidogo.”
Wabunge
wa Upinzani wamekuwa na tabia ya kususa vikao vya Bunge mara kwa mara kutokana
na madai mbalimbali, hali ambayo sasa imeanza kuzoeleka miongoni mwa Bunge na
jamii ya Tanzania.
Kuhusu
suala la IPTL, Waziri Mkuu aliwataka wabunge kuheshimu mamlaka ya CAG kwani
imeundwa kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania Ibara ya 143.
“Kwa
kweli ofisi hii tunaitegemea sana na isianze kujengeka dalili kuwa pengine
hatuna imani na chombo hiki. Hii itatuletea tabu.
“Tumewakabidhi
jukumu wenzetu wafanye kazi na kisha watatuletea majibu kama kuna mgogoro ama
ubadhirifu au rushwa,” alisema Waziri Mkuu.
Kwa
mujibu wa Bunge, Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali (PAC), iliagiza CAG kwa
kushirikiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kufanya
uchunguzi kwenye malipo ya IPTL katika akaunti ya Escrow ya Benki Kuu (BoT).
Hiyo
imetokana na kuwapo tuhuma kwamba fedha hizo zimechukuliwa kinyume cha
utaratibu, jambo ambalo Serikali imesema hakuna kilichokiukwa.
Waziri
Mkuu aliahidi kuwa baada ya uchunguzi, Serikali haitakuwa na kigugumizi katika
kuchukua maamuzi kwa wote ambao watakuwa wameonekana kuguswa na suala hilo bila
kujali nyadhifa zao.
“Tutachukua
hatua stahili baada ya uchunguzi huu, lakini kwa sasa suala hili ni tuhuma tu
na isingefaa kuwashutumu watu. Tena wakati tukiambiwa kuwa ushahidi ulioletwa
hapa, makaratasi mengine hayana kitu,” alifafanua Waziri Mkuu.
Akihitimisha
mjadala wake, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alieleza
kwa kina kuhusu suala la kampuni hiyo ya kufua umeme tangu lilipoanza mwaka 1998.
Kwa
mujibu wake, fedha hizo zinazolalamikiwa hazikuwa mali ya umma na kwamba
zilihifadhiwa kwa mujibu wa amri ya Mahakama kusubiri mzozo wa wamiliki wake.
Alisema
Serikali imepata fedha zake kwa mujibu wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).
Naye
Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM), alisisitiza kuwa alichonacho mbunge
mwenzake, Christopher Sendeka kuwa nyaraka za ushahidi wa sakata la IPTL, ni
sawa na makaratasi ya kufungia maandazi, kwani hayana uhalali.
“Nataka
kuweka kumbukumbu sahihi na katika Hansard (Taarifa Rasmi za Bunge). Mheshimiwa
Sendeka amelalamika kwa mimi kusema kwamba aliyonayo ni makaratasi ya kufungia
maandazi.
“Kwa
mujibu wa sheria, hati unapaswa kuwa nazo kama wewe ni custodian (Mwangalizi)
wake, siyo kuwa na photocopy sijui za IPTL, nyingine za Hong Kong, na Tanesco.
Hizi hazina authentic (uhalisia). Atulie. Hizi ni sawa na makaratasi ya
kufungia maandazi kule kwenye mgahawa jimboni kwangu. Angesema ana taarifa
ningeelewa, lakini siyo ushahidi,” alisema Lugola.
Katika
hatua nyingine, Waziri Mkuu Pinda amesema Serikali italiangalia ukweli wa
tuhuma zinazomkabili Balozi wa Uingereza nchini, Diana Malrose.
Juzi,
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Stephen Masele akichangia hoja ya bajeti ya
wizara hiyo, alimtuhumu Malrose kuingilia masuala ya ndani ya Tanzania kinyume
cha Mkataba wa Vienna kuhusu masuala ya kidiplomasia na kumtaka ajipime kama
anafaa kuendelea kuiwakilisha nchi yake hapa nchini.
Waziri
Mkuu Pinda alisema amelisikia jambo hilo na kwamba Serikali italiangalia kuhusu
ukweli wake na kuona kinachohitajika kufanyika.
>>Habari Leo
>>Habari Leo
Post a Comment